FAHAMU HUDUMA YA UTOAJI MAPEPO (EXCORCISM) KATIKA KANISA KATOLIKI.
Na


Wilehard Maro
Niliye mdogo kuliko wote.
Lipo swali au shutuma juu ya kanisa katoliki kuwa “wakatoliki hawatoi mapepo kama alivyofanya Yesu” basi leo tuichambue huduma hii katika kanisa katoliki. Kwanza ni wazi kuwa kanisa katoliki linatoa huduma hii kwa waamini wanaothibitika kushikiliwa na nguvu za kishetani (demonic possession) kwa kuondoa nguvu hizo kwa jina la Yesu. Katekisimu ya Kanisa Katoliki namba 1673 inaeleza kuwa kupunga pepo kunaelekezwa katika kumfukuza shetani au ukombozi dhidi ya kupagawa na pepo na kupitia kwa mamlaka ya kiroho ambayo Kristo amelikabidhi Kanisa. Mara nyingi huduma hii haifanyiki kwa uwazi au mbele ya kusanyiko kama ilivyo kwa baadhi ya madhehebu ya kipentekoste na kiprotestanti hivo kufanya ionekane kama huwa haifanyiki lakini ni kweli kuwa huduma hii inafanyika ndani ya kanisa katoliki.

1.      Kupunga pepo kulianza lini?
Visa vya kupunga pepo ni vya zamani kabla na baada ya Yesu, ila katika utaratibu wa kanisa, mwaka 1614, kanisa lilitoa mingozo rasmi juu ya upungaji pepo. Karne ya 15, walei na mapadre walipunga pepo, wote walihesabiwa kuwa wana nguvu na mamlaka hayo na njia ya Kibenectine iliyojilikana kama  "Vade retro satana" ilitumiwa kwa lugha yetu “rudi nyuma, shetani”. Mwaka 1999 miongozo hiyo ya upungaji pepo ilipitiwa upya kutokana na kuongezeka kwa mahitaji. Utaratibu huo ulitolewa kuweka maelekezo ya namna ya mtu anayedai kuwa na mapepo atafwata ili kupata huduma hii, ikijumuisha uchunguzi wa kitabu unaofanywa na wataalamu wa magonjwa ya akili.
2.      Nani anatoa mapepo?
Ni muhimu kutambua kuwa huduma hii ni ya masakramenti ila si sakramenti (sacramental but not a sacram). Hivyo kanisa limeelekeza wazi kwa sheria zake (canon law) namba 1172 namba mbili kinaleza Padre mwenye uelewa na elimu ya nguvu hizo anaruruhisiwa kufanya huduma ya kupunga pepo kwa ruhusa ya askofu wa Jimbo lake. Pia sharia hii inkatza katika kifungu namba moja kuwa hakuna mtu mwengine anaruhusiwa ispokuwa Padre. Hivyo ni wazi kuwa huduma hii inatolewa na wenye daraja tu, waumini wa kawaida hawaruhusiwi.  Mkuu wa Idara Idara ya Ibada Takatifu na Masakramenti Kardinali Jorge Arturo Medina Estevez anasisitza ya kuwa "Kuendesha ibada hiyo ya kupunga mashetani," anakazia, "lazima kuthibitishwe na kukubaliwa na Askofu wa Jimbo, ambako kunaweza kutolewa kwa tukio maalum, au kwa njia ya kudumu kwa Padre aliye na huduma ya kupunga mashetani Jimboni."

3.      Nani anapungwa mapepo.
Utaratibu wa kupunga mapepo umewekwa na kanisa ili kutobebesha mzigo wagonjwa au watu wenye matatizo ya kiakili kwenye huduma hii badala yake, wapate tiba za kitabibu. Kutokana na uchache wa kesi za kweli, miongozo ya Vaticani ya mwaka 1999 inaeleza wazi kuwa lazima madaktari wathibitishe kuwa mtu huyo hana matatizo yoyote ya afya ya akili. Matatizo ya kimaisha, uchumi, mahusiano, afya, jamii, siasa na mengineyo yanayowazonga wengi yanapelekea msongo wa mawazo na kufanya watu wengi kutawaliwa na hisia mbaya na matatizo ya kiakili. Waafrica wengi wanatawaliwa na woga dhidi ya uchawi na mara kadhaa wanapojikuta katikati ya msongo wa mawazo na mara moja hofu ya uchawi inaingia na kujitengenezea akili kuwa wanatekwa na nguvu za kipepo. Lakini kanisa linataka kuthibishwa kwa nguvu za kipepo kabla ya huduma hii. Hivyo, anayethibitika tu ndiye atakayepewa huduma.

4.      Je zipo dalili za kuweza kuashiria mtu mwenye kuweza kuwa na mapepo?
Mtandao wa Wikipedia unataja baadhi ya dalili ambazo si za kawaida na kama mtu anazo baadhi au zote basi vyema kuangalia utaratibu jimboni kwako kupata huduma hii. Kuna kukosa au kutokuwa na hamu ya kula, kujikatakata au kujichubua au kujing’ata Ngozi, kuhisi chumba ni cha baridi, mabadiliko yasiyo ya kawaida ya mwili na uso na mikao isiyo ya kawaida, kupoteza uwezo wa kujimiliki na kushambulia wengine, kutoa sauti za ajabu, nguvu za ajabu au zisizo za kawaida, kuongea na kuelewa lugha ambayo muhusika hajawahi kuijua kabla, ufahamu wa vitu ambavyo vimefichwa au kutoonekana, kutabiri mambo ya badae, Chuki kubwa dhidi ya vitu vyote vya kidini, kupata shida kuingia kanisani au kusikia neno Yesu, kufukuza vitu au Wanyama. Zingatia kuwa kuwa na dalili moja si kigezo kamili na hata ziwepo basi ni padre mwenye ruhusa ndiye atakayechukua jukumu la kuthibitisha au kukataa.

5.      Mchakato wa utoaji mapepo.
Kwanza muhusika atafungwa au kuweka mahala ambapo hataweza kuwadhuru wengine au yeye mwenyewe kisha, padre atafanya sala kumtoa mtu huyo mapepo. Muongozo wa kotoa mapepo unapatikana katika hati ya vatikani ya  De Exorcismis et Supplicationibus Quibusdam na pia katika  ibada cha madhehebu ya Kirumi. Mchatako huu huenda usifanikiwe mara moja, bali kwa siku, wiki n ahata mwezi kwa muendelezo wa sala ya kupunga pepo.
Kila jimbo lina uwezekano wa kuwapo kwa padre mpunga mapepo hivyo waamini wanaodhani kuwa wanahitaji basi wakaribie kuitafuta na ni vyema sana kukubali pale unapothibitika una matatizo ya kiakili si mapepo. Tabia ya baadhi ya waamini kupunga mapepo si nzuri ni kinyume na taratibu na ni wazi kesi nyingi za waamuni kutoa mapepo zinajikita katika woga wa kurithi na matatizo ya msongo wa mawazo. Wanaoweza kuingiwa pepo ni wale wasioungama kabisa, hawashiriki wala kutaka kushiriki sakramenti za kanisa, pepo hawawezi muingia mtu msafi bali wanafuata mahali wanapoweza kuishi. Silaha kubwa dhidi ya mapepo ni kuishiriki vyema sakramenti ya kitubio, kusali mara kwa mara, kutumia vitu vyenye baraka, kupokea ekarist takatifu mara kwa mar ana kuishi usafi wa moyo. Mapepo kumuingia mkristo si jambo jepesi kama tunavyoweza kusikia au kuona kwa watu wengine. Katika mada hii, jiulize tu, kwa nini wanaotolewa mapepo huko kwengine ni watu wa kipato cha chini, historia za kukandamizwa na wanatokea kwenye jamii zenye kuamini ushirikina, kamwe mama matajiri, watu wenye amani nautulivu huwakuti kwenye vurumai hizi? Lipo swala ambalo kanisa liliona na kuweka utaratibu, wengine wanahitaji tu kupatanishwa na ndugu zao wala si kuombewa kwani wanaishi na chuki moyoni, wengine wana msongo wa mawazo na hawana ahueni. Yote haya ni matatizo tunayobakizia huduma hii wakati huduma za ushauri toka kwa wataalamu ungetatua matatizo hayo.
Basi nawatakieni kila jema katika kujilinda na upotofu wa sasa, na vyema sana waamini walei kuongeza bidi ya kujifunza na kuchimba mafundisho badala ya kuketi tu tukilalama kanisa limekosa hiki ama kile. Tuwaone mapadre pia kwa maelekezo mazuri. Asanteni.


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

Biblia ni nini? Asili, Historia, waandishi na mipaka yake

HISTORIA YA HAYATI BABA WA TAIFA MWL. JULIUS NYERERE